Upungufu wa madawati ubovu wa majengo wakwamisha masomo Ng’ahelezi
24 August 2026, 17:08

Mwenyekiti wa Kijiji cha Ng’ahelezi, Msafiri Chahonza, amekiri kuwepo kwa changamoto ya upungufu wa madawati, majengo ya madarasa na idadi ndogo ya walimu, huku akiiomba Serikali kuongeza madawati, kuboresha miundombinu na kupeleka walimu wa kutosha wa jinsia zote ili kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji katika shule hiyo.
Na Victor Chigwada
Wanafunzi wa Shule ya Msingi Ng’ahelezi wanakabiliwa na changamoto ya upungufu wa madawati, majengo ya madarasa na uchakavu wa baadhi ya miundombinu, hali inayowaathiri katika mazingira ya kujifunzia, hususan wakati wa msimu wa mvua.
Wakizungumza kuhusu hali hiyo, baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Ng’ahelezi wamesema msimu wa mvua umekuwa changamoto kubwa kwa wanafunzi, kwani baadhi yao hulazimika kusoma katika mazingira yasiyo salama na kulowanisha madaftari yao kutokana na uchakavu na upungufu wa madarasa.
Aidha, wakazi hao wamesema mazingira yasiyoridhisha ya shule yanaathiri usafi, usalama na umakini wa wanafunzi katika kujifunza, hivyo kuhitajika hatua za haraka kuboresha miundombinu ya shule hiyo.