Umbali wa shule wahatarisha usalama wa wasichana Chisichili
20 August 2026, 16:36

Hata hivyo, jamii inapaswa kuendelea kujenga mazingira rafiki na salama kwa watoto wa kike, huku ikitafuta njia mbadala na za kudumu zitakazowahakikishia utulivu katika masomo yao bila hofu yoyote.
Na Derrick Mazembe.
Safari ya kutafuta elimu kwa watoto wakike, hasa wale wanaolazimika kutembea umbali mrefu kwenda shuleni, imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali.
Hali hii imeibua mjadala mpana kuhusu usalama wa mazingira yanayowazunguka na jinsi yanavyoweza kuathiri ushiriki na ufaulu wao katika masomo, pamoja na vishawishi mbalimbali wanavyo kumbana navyo.
Mtaa wa Chisichili unaopatikana katika kata ya Matumbulu Jijini Dodoma ni moja ya maeneo yanayo kumbwa na adha ya ukosefu wa shule karibu hivyo wanafunzi wa eneo hilo hulazimika kutembea umbali mrefu kila siku kwaajili ya kwenda shuleni.
Wananchi hao wanasema usalama wa watoto wao hasa wakike umekuwa hatarini kwani wanakutana na vishawishi mbalimbali njiani na wakati mwingi hukumbna na vitendo vya ukatili.
Mwenyekiti wa eneo hilo Bw. John Wami amekiri kuwepo kwa changamoto hiyo ambapo amesisitiza umuhimu wa wazazi na jamii kushirikiana kwa ukaribu ili kuhakikisha ulinzi thabiti unakuwepo kwa wanafunzi wa kike wakati wote wanapokuwa nje ya mazingira ya nyumbani na shuleni.
Stephen Noel ni Mratibu wa Mtandao wa Marafiki Elimu yeye amewataka wadau wa elimu na serikali kuangalia namna ya kuboresha miundombinu, ikiwemo ujenzi wa mabweni au kuweka mipango ya usafiri salama, badala ya kuwaacha wanafunzi wakitembea umbali mrefu kufuata shule.