

17 April 2025, 5:59 pm
Miradi hiyo itasaidia kuongeza hali ya uzalishaji maji huku akisema zaidi ya Bilioni 3 zimetumika kutekeleza mradi wa maji Nala.
Na Mariam Kasawa.
Waziri wa Maji Mhe Juma Aweso amewataka watumishi wa Wizara hiyo kuhakikisha wanaishirikisha jamii wanapofanya tafiti za kina za kugundua vyanzo vipya vya maji.
Aweso ametoa kauli hiyo leo jijini Dodoma wakati wa Ziara ya kukagua miradi ya Maji inayosimamiwa na Mamalaka ya Maji safi na usafi wa mazingira Dodoma (DUWASA) katika eneo la Nala, Chihoni.
Kwa upande wake Mbunge wa Dodoma Mjini na Waziri wa Madini Mhe Antony Mavunde amesema kukamilika kwa miradi ya uchimbaji wa visima vya maji pembezeno mwa mji itasaidia kuongeza hali ya upatikanaji wa maji katika maeneo ya Nala,Chihoni,Segu na maeneo ya Viwanda.
Awali akisoma taarifa ya Miradi ya maji ya Nala na Amani Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira Dodoma [DUWASA] Mhandisi Aron Joseph amesema miradi hiyo itasaidia kuongeza hali ya uzalishaji maji huku akisema zaidi ya Bilioni 3 zimetumika kutekeleza mradi wa maji Nala wakati Bilioni 41 kwenye Mradi wa uchimbaji wa visima vya maji pembezoni mwa mji katika eneo la Amani.
Nao baadhi ya wananchi wameishukuru Serikali kupitia Mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira DUWASA kwa kuwachimbia visima hivyo vya maji kwani awali kabla ya uwepo wa miradi hiyo kutekelezwa katika maeneo hayo walikuwa wanatumia muda mrefu kutafuta huduma ya maji safi na salama.