Dodoma FM

Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania mh. Samia Suluhu asema mamlaka za serikali za mitaa ni nguzo muhimu kwa Taifa

27 September 2021, 12:30 pm

Na; Fred Cheti.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.Samia Suluhu Hassani leo Septemba 27 ameshiriki mkutano wa jumuiya ya tawala za mikoa Tanzania(ALAT) ambao ni maalumu kwa ajili ya uchaguzi wa mamalaka hizo.

Akizungumza katika mkutano huo uliofanyika jijini Dodoma katika ukumbi wa Jakaya Kikwete Rais Samia amesema kuwa mamlaka za serikali za mitaa ni nguzo muhimu kwa taifa na ni injini ya maendeleo nchini kwa kuwa zipo karibu zaidi na wananchi.

Aidha Rais Samia amewataka viongozi hao wa Mamlaka za serikali za Mitaa (ALAT ) pamoja na madiwani wote nchini watakaochaguliwa kuongoza katika miaka mitano ijayo kuyapa kipaumbele mambo kadhaa ikiwemo kuendeleza kazi za ALAT kama zilivyo kisheria.

Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.Kasimu Majaliwa ni miongoni mwa viongozi waliohudhuria mkutano huo ambapo ameipongeza Wizara ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na serikali za Mitaa (TAMISEMI) inayosimamia mamlaka hizo kwa kazi nzuri inayofanya ya kuwahudumia wananchi

Mkutano huo ambao ni maalumu kwa ajili ya uchaguzi wa viongozi wa mamlaka za serikali za mitaa unatarajia kufanyika kwa siku mbili kuanzia leo septemba 27 hadi septemba 29 na Kauli mbiu katika mkutano huo ni” CHAGUA VIONGOZI BORA KWA MAENDELEO ENDELEVU”