Dodoma FM

Vijana miaka 13 hadi 35 wahanga matumizi ya dawa za kulevya

22 June 2026, 16:18

Picha ni Afisa Mwandamizi kutoka Mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya Anna Tenga.Picha na Dodoma live.

Siku ya Kimataifa ya Kupiga Vita Dawa za Kulevya Duniani huadhimishwa kila mwaka tarehe 26 Juni.

Na Elizabeth Tanzania

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Tanzania (DCEA) imeeleza kuwa matumizi ya dawa za kulevya ni changamoto kubwa  na kundi la vijana wenye umri kati ya miaka 13 hadi 35 ndilo huathirika zaidi.

Akizungumza na Taswira ya Habari,Afisa Mwandamizi kutoka Mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya Anna Tenga amesema katika kundi hilo la vijana wengi wao wapo kwenye ngazi ya elimu ya msingi,sekondari,vyuo vya kati hadi vyuo vikuu na wasio katika mfumo rasmi wa elimu.

Amesema kuelekea maadhimisho ya siku ya kimataifa ya kupiga vita matumizi ya dawa za kulevya Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya wameendaa bonanza la michezo kwa vijana mbalimbali kwa lengo la kuendelea kutoa elimu kwa jamii juu ya madhara yatokanayo na matumizi ya dawa za kulevya.

Sauti ya Anna Tenga.

Ameongeza kuwa ni lazima jamii kusimama na kupiga vita matumizi ya dawa za kulevya kwani madhara yake ni makubwa ikiwemo kuwa na jamii ya watu wenye vitendo vya ukatili.

Sauti ya Anna Tenga.

Siku ya Kimataifa ya Kupiga Vita Dawa za Kulevya Duniani huadhimishwa kila mwaka tarehe 26 Juni ambapo kwa mkoa wa Dodoma maadhimisho hayo yatafanyika katika chuo kikuu cha St. John yakiwa na kauli mbiu “Ubunifu wa kimkakati -Suluhisho la changamoto ya dawa za kulevya” na mgeni rasmi akitarajiwa kuwa mkuu wa mkoa wa Dodoma Mh. Rosemary Senyamule.