Dodoma FM
Dodoma FM
5 May 2026, 15:32

Katika hatua ya mwisho ya ukaguzi huo, Kamati ya TAMISEMI ilitoa mapendekezo mbalimbali ya kuboresha utekelezaji wa mradi huo wa usalama wa kidijitali.
Na Anwary Shaban.
Katika muendelezo wa ziara ya kamati ya kudumu ya Bunge TAMISEMI, 2026 , imetembelea na kukagua mradi wa ufungaji wa kamera za ulinzi(CCTV Camera) unaotekelezwa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika maeneo ya katikati ya Jiji hilo.
Akizungumza wakati wa kikao cha majumuisho mara baada ya ukaguzi wa mradi huo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, alisema Mkoa umefanya tathmini ya kina na kuamua kuwekeza katika mifumo ya kidijitali ili kulinda Viongozi, Wawekezaji na Wananchi na mali zao.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri, aliipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya Umma ikiwemo barabara za pete (mzunguko), treni ya kisasa ( SGR) pamoja na majengo ya kisasa ya ofisi za Serikali, akieleza kuwa ni wajibu wa mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha miundombinu hiyo inalindwa ipasavyo.

Katika hatua ya mwisho ya ukaguzi huo, Kamati ya TAMISEMI ilitoa mapendekezo mbalimbali ya kuboresha utekelezaji wa mradi huo wa usalama wa kidijitali, ili ulete tija,na thamani ya fedha iliyotumika iweze kuonekana, ambapo Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeyapokea, na kuahidi kuyafanyia kazi kwa ufanisi ili kuimarisha zaidi usalama na kulinda mafanikio ya uwekezaji wa miundombinu ndani ya Jiji hilo.