Dodoma FM

Wakazi wa Mloda watatuliwa kero ya maji iliyo dumu kwa muda mrefu

3 September 2021, 12:32 pm

Na; Selemani Kodima.

Uongozi wa kijiji cha Mloda Wilayani Chamwino umesema maisha ya wakazi wa kijiji hicho yameanza kubadilika baada ya kutatuliwa changamoto ya kisima cha maji ambayo imewatesa kwa muda mrefu.

Akizungumza na Taswira ya Habari Mwenyekiti wa Kijiji cha Mloda Bw. Adam Anorld amesema ni miezi miwili imepita tangu wamechimbiwa kisima cha maji hali ambayo imeleta faraja katika maisha ya wakazi wa eneo hilo katika utafutaji wa huduma ya maji.

Amesema kitendo cha maji kuwa karibu na wananchi kimeondoa malalamiko ya mara kwa mara kuhusu changamoto hiyo.

Kwa upande mwingine Uongozi huo wameiomba Serikali kuwachimbia kisima cha Maji baridi kutokana na maji wanayotumia kuwa na wingi wa chumvi .

Pamoja na hayo Mwenyekiti huyo amewataka wananchi kuwa na subira wakati wakiendelea kutumia maji yanayopatikana kwa sasa kwa kuzingatia matumizi sahihi .