Dodoma FM

Wanaume wanawezaje kuripoti matukio ya ukatili wa kijinsia?

7 August 2026, 12:52

Idadi ya wanaume wanaofanyiwa vitendo vya ukatili imekuwa ikiongezeka katika miaka ya hivi karibuni.Picha na Mtandao.

Ni muhimu kufahamu kuwa ukatili umegawanyika katika makundi manne makuu: ambayo ni ukatili wa kimwili, ukatili wa kingono, ukatili wa kihisia na ukatili mwingine.

Na Mariam Kasawa.
Ukatili wa kijinsia ni kitendo chochote cha unyanyasaji ambacho husababisha, au kinaweza kusababisha madhara ya kimwili, kihisia, kiakili au mateso kwa mhanga wa tukio la ukatili.

Ni muhimu kufahamu kuwa ukatili umegawanyika katika makundi manne makuu: ambayo ni ukatili wa kimwili, ukatili wa kingono, ukatili wa kihisia na ukatili mwingine.

Aina hizi za ukatili zinajumuisha makosa kama kubaka, kulawiti, shambulio la aibu, mauaji, mauaji ya vikongwe kwa imani za kishirikina, kujeruhi, kukeketa, shambulio, na kutupa watoto.

Nyingine ni wizi wa watoto, usafirishaji haramu wa binadamu, kutelekeza familia, kupoka, kuzorotesha masomo ya mwanafunzi na ndoa za utotoni.

Takwimu za bajeti ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maalum ya mwaka 2025/26 zinaonesha kuwa katika kipindi cha Julai 2024 hadi Aprili 2025 jumla ya manusura wa ukatili 19,717 waliripotiwa nchini Tanzania.

Kati ya manusura hao, wanaume ni 4,472 sawa na asilimia 22.6 au karibu robo ya manusura wote walioripotiwa katika kipindi hicho cha miezi 10.

Licha ya kuwa ukatili wa kijinsia huwakumba zaidi wanawake, idadi ya wanaume wanaofanyiwa vitendo hivyo imekuwa ikiongezeka katika miaka ya hivi karibuni, jambo linaloibua maswali mengi kuhusu hatma yao.

Ripoti ya Takwimu za Unyanyasaji na Ukatili wa Kijinsia ya 2024 iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani, Jeshi la Polisi na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum inaonesha kuwa mwaka 2023 wanaume 12,028 waliripotiwa kufanyiwa ukatili wa kijinsia.