Dodoma FM

Plan International yazindua girls take over, sikia sauti zetu

27 September 2024, 6:00 pm

Mkurugenzi Mkazi wa Plan International Bi. Jane Sembuche (mwenye miwani katikati) akielezea kampeni za girls take over na sikia sauti zetu kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam. Picha na Hilali Ruhundwa

Oktoba 11 kila mwaka dunia huadhimisha Siku ya Kimataifa ya Msichana lengo likiwa ni kutoa elimu juu ya umuhimu wa upatikanaji wa haki na uwezeshaji wa wasichana duniani kote.

Na Hilali Ruhundwa

Kuelekea Siku ya Msichana Duniani, shirika la Plan International limezindua kampeni mbili kimataifa za girls take over (wasichana kushika hatamu) na sikia sauti zetu (hear our voices) zikilenga kuleta mabadiliko ya kijamii katika uongozi ili kuondoa vikwazo, ubaguzi na dhana potofu zinazoendelea kuwazuia wasichana kufikia ndoto zao.

Akielezea kampeni hizo kwa waandishi wa habari, Mkurugenzi Mkazi wa Plan International Bi. Jane Sembuche amesema kuwa katika jamii nyingi msichana amekuwa akinyimwa haki ya kufikia ndoto zake tofauti mvulana.

Bi. Jane Sembuche akielezea kampeni ya girls take over

Kampeni ya girls take over inazinduliwa kwa miaka mingine mitatu na imekuwa msaada mkubwa kwa kuondoa vikwazo vya wasichana kufikia ndoto zao. Felister Alex ni mmoja wa wasichana walionufaika na kampeni hiyo.

Sauti ya Felister Alex mnufaika wa kampeni ya girls take over
Felister Alex mnufaika wa kampeni ya girls take over. Picha na Hilali Ruhundwa

Kwa upande wake Jacqueline Mtamya ambaye amenufaika na kampeni hiyo mwaka 2022, amesema kuwa tangu ajiunge na kampeni hiyo amekuwa balozi mzuri wa kupambania wasichana kufikia malengo yao ambapo kwa sasa ni mwakilishi wa kampeni hiyo katika nchi za Mashariki ya Kati.

Jacqueline Mtamya (katikati) akielezea manufaa ya kampeni ya girls take over ilivyomsaidia. Picha na Hilali Ruhundwa

Akizungumzia kampeni ya sikia sauti zetu, Mkurugenzi Mkazi wa Plan International Bi. Jane Sembuche amesema kuwa kampeni hiyo inalenga kutatua changamoto za msichana hasa suala la ndoa na mimba katika umri mdogo.

Aidha Bi. Sembuche amesema sheria ya ndoa ya Tanzania ya mwaka 1971 vifungu vya 13 na 17 ni vema vibadilishwe ili kuwalinda watoto wa kike nchini. Amesema kuwa hali ya ndoa za utotoni inasikitisha sana ambapo wasichana 3 kati ya 10 huolewa kabla ya kufikisha umri wa miaka 18 huku asilimia 28 ya wanawake nchini wakifanyiwa ukatili wa kingono wakati wa utoto, hii ikiwa ni kwa mujibu wa Ripoti ya UNICEF 2023.

Bi. Jane Sembucha akielezea changamoto ya sheria ya ndoa nchini ya mwaka 1971

Zafarani Ramadhani ni mhitimu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam shahada ya kemia anaeleza kuwa alizaliwa katika familia isiyo na uwezo wa kumwezesha kufikia ndoto zake lakini baada ya kupata nafasi kupitia kampeni ya girls take over anaona ndoto zake zinatimia.

Sauti ya Zafarani Ramadhani
Mariam Albhai Surve mnufaika wa kampeni ya girls take over. Picha na Hilali Ruhundwa

Kwa upande wake Mariam Albhai Surve ambaye ni afisa tabibu na mchechemuzi wa afya ya akili, anakiri kwamba mazingira duni ya familia na jamii yake yalimfanya kupoteza matumaini ya kufikia malengo yake lakini kwa sasa anauona mwanga.

Sauti ya Mariam Albhai Surve

Shirika la Plan International limekuwa msaada kwa wasichana katika kufikia malengo yao hasa katika kuleta usawa kwenye elimu, uongozi na afya.