Dodoma FM

‘Jamii ibadili mitazamo ukatili wa kijinsia’

10 April 2025, 5:57 pm

Dkt. Jingu amewataka wadau hao kuongeza ufanisi na ufatiliaji wa programu hiyo ili kuweza kutimiza malengo yaliyodhamiriwa toka kuazishwa.Picha na Maendeleo ya jamii.

Utekelezaji wa Programu ya mabadiliko na Kupinga Ukatili wa kijinsia (GTAP) iliyoanza mwaka 2022/2023 unatarajia kukamilika 2025/2026.

Na Mariam Matundu.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. John Jingu ameitaka jamii kubadilika na kuachana na dhana ya kumdidimiza mtoto wa kike kwani dhana hiyo ni kikwazo cha maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Dkt. Jingu ameyabainisha hayo katika kikao kazi baina ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Wizara za kisekta zinazoratibu Kupinga Ukatili wa kijinsia (GTAP) na Umoja wa Ulaya kilichofanyika jijini Dodoma Aprili 09, 2025.

Dkt. Jingu amewataka wadau hao kuongeza ufanisi na ufatiliaji wa programu hiyo ili kuweza kutimiza malengo yaliyodhamiriwa toka kuazishwa kwake ikiwemo kupunguza vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto, kwainua wanawake kiuchumi na kuhakikisha mabinti wanarudi shule.

“Tunaweza kujifunza mifano mizuri kutoka kwa walioweza kudhibiti wanaokinzana na sheria na taratibu za nchi hii kwa kufuata nyanyo zao ili jamii iweze kutambua kuwa endapo mtu atakiuka taratibu zilizopo atachukuliwa hatua stahiki ikiwemo kifungo kwani majadiliano si suluhu ya kila kitu muda mwingine hatua kali ni muhimu “amesema Dkt Jingu.

Aidha Dkt. Jingu amepongeza hatua zilizofikiwa toka kuanzishwa kwa utekelezaji wa programu hiyo nchini ikiwemo kuongezeka kwa idadi ya mabinti walioweza kurejea shuleni baada ya kukatishwa masomo, kuongezeka kwa nyumba salama kwa manusra wa ukatili lakini pia asilimia kubwa ha wanajamii kuamka na kuanza kuachana na vitendo vya ukatili.

Serikali itaendeleza kuweka juhudi na afua mbalimbali ili kuhakikisha wanawake wanaendelea kuwa salama .Picha na Maendeleo ya jamii.

Kwa upande wake Mwakilishi kutoka Umoja wa Ulaya Karina Dzialowska ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano wake na Umoja wa Ulaya katika kutengeneza mazingira salama na rafiki kwa mtoto wa kike kuweza kustawi na kuweza kufikia malengo yake.

“Tunatarajia hata baada ya programu hii kuisha Serikali itaendeleza kuweka juhudi na afua mbalimbali ili kuhakikisha wanawake wanaendelea kuwa salama kwani bado kuna safari ndefu ya kuhakikisha watoto wa wanaondokana na vitendo vya ukatili wa kijinsia” amesema Dzialowska.