Dodoma FM

Zao la zabibu kuanza kutangazwa nchini Burundi

17 February 2026, 4:47 pm

Picha ni Balozi wa Tanzania nchini Burundi Mhe. Gelasius G. Byakanwa akiwa na mkuu wa mkoa wa Dodoma Mh.Rosemery Senyamule.Picha na Mkoa wa Dodoma.

Nao, baadhi ya wachakataji na wazalishaji wa mvinyo, wamefurahia fursa hiyo na kumhakikishia Balozi kwamba watashiriki maonesho hayo na kusema kuwa watajitahidi kuzalisha bidhaa zenye ubora na viwango vya kimataifa .

Na Mariam Kasawa.

Balozi wa Tanzania nchini Burundi Mhe. Gelasius G. Byakanwa, amefanya kikao na wazalishaji na wachakataji wa zao la Zabibu wanaozalisha Mvinyo (Wine) Mkoa wa Dodoma akilenga kutangaza bidhaa hiyo nchini Burundi ambayo ni ya kipekee kuzalishwa nchini Tanzania katika Mkoa wa Dodoma Februari 16,2026.

Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Jengo la Mkapa Jijini hapa ambapo Mhe. Balozi Byakanwa amesema anaandaa maonesho ya Mvinyo unaozalishwa Dodoma nchini Burundi mwezi Mei, 2026, ambapo wachakataji hao watapata fursa ya kutangaza soko lao nchini humo.

Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule, amepongeza jitihada za Balozi huyo kutangaza soko la Mvinyo nchini Burundi na kusema kuwa hatua hiyo itakwenda kumaliza kabisa changamoto ya upatikanaji wa soko la zabibu hususan kinywaji adhimu cha Mvinyo kwani Dodoma imekua na uzalishaji mkubwa lakini soko ndio limekua si la uhakika.

Sauti ya Mhe. Gelasius G. Byakanwa, na Senyamule.