Dodoma FM

Wanawake na wanaume wanategemeana katika kuleta maendeleo

2 September 2024, 5:01 pm

Picha ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima wakati akifungua mkutano wa kwanza wa mtandao wa wanawake wa Jeshi la Magereza nchini.Picha na Maendeleo ya Jamii.

Na Mariam Matundu.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima amesema wanawake na wanaume wanategemeana katika kazi ili kuleta maendeleo endelevu.

Waziri Dkt. Gwajima amesema hayo wakati akifungua mkutano wa kwanza wa mtandao wa wanawake wa Jeshi la Magereza nchini, uliofanyika Septemba 02, 2024 jijini Dodoma.

Waziri Dkt. Gwajima amebainisha kwamba, hali hiyo ya kutegemeana inatokana na tofauti ya utekelezaji wa majukumu katika maeneo mbalimbali kati ya mwanamke na mwanaume ambapo husababisha wanawake kupewa msukumo wa kipekee katika kuhakikisha majukumu ya familia hayaathiri ushiriki wao katika nafasi za maamuzi na Ujenzi wa Taifa.

Amesema Sera hiyo imeweka mazingira wezeshi kwa wanawake na wanaume katika kutekeleza majukumu yao kulingana na mahitaji ya kijinsia.

Aidha Waziri Dkt. Gwajima amemuomba Kamishna Jenerali wa Magereza kuangalia namna ya kujenga vyumba vya kunyonyeshea watoto mahali pa kazi katika miundombinu mipya ya Magereza, ikiwa ni mpango pia wa Serikali katika kusaidia afya za watoto na akina mama kupata utulivu ili kutekeleza majukumu yao.

Picha ni Kamishina wa Huduma za Urekebu na Mwenyekiti wa mtandao wa wanawake wa Jeshi la Magereza Taifa Bertha Minde .Picha na Maendeleo ya jamii.

Amebainisha kuwa kufurahishwa na uanzishwaji wa mtandao huo wa wanawake wa Jeshi la Magereza kuwa ni majibu ya matokeo ya kazi anazozifanya na Wizara anayoiongoza, hasa kwa namna gani Sera na Miongozo inayotolewa katika kufikia usawa wa kijinsia kwenye nyanja mbalimbali nchini zinatekelezwa kwa vitendo.

Kwa upande wake Kamishina wa Huduma za Urekebu na Mwenyekiti wa mtandao wa wanawake wa Jeshi la Magereza Taifa Bertha Minde amesema, baadhi ya malengo la mtandao huo ni kuongeza ufanisi wa kazi, kutambua mchango wa wanawake jeshini, kuleta usawa wa kijinsia katika utekelezaji wa majukumu na kusaidiana na jamii katika kupunguza uhalifu kwenye jamii.

Naye Makamu Mwenyekiti wa mtandao huo Sp Tekla Ngilangwa, akisoma risala ya mtandao huo, amebainisha kwamba Mtandao wa Wanawake wa Jeshi la Magereza ulioanzishwa mwaka 2018 ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya Kikao cha Kamati ndogo ya Wakuu wa Magereza wa nchi za SADC uliofanyika Lusaka – Zambia mwaka 2011 ambapo kwa upande wa Jeshi la Magereza nchini, utekelezaji wa azimio hilo ilikuwa ni kuendeleza mikakati iliyopo kwenye Sera ya Maendeleo ya Wanawake iliyoanza kutumika mwaka 1992 na Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia ya mwaka 2000