Dodoma FM
Dodoma FM
6 February 2026, 12:48 pm

Hatua ya Shirika la Posta Tanzania kuanza kutumia wataalam wa lugha ya alama inatajwa kuwa mfano wa kuigwa kwa tasisi zingine za umma katika kuhakikisha haki ya kupata huduma inazingatia kila mwananchi bila ubaguzi.
Na Anwary Shaban.
Shirika la Posta Tanzania limepanga kuanza kutumia wataalam wa lugha za alama katika vituo vyake vya huduma nchini ikiwa ni sehemu ya juhudi za serikali kuhakikisha watu wenye mahitaji maalumu hawabaki nyuma katika maendeleo ya huduma za kidigitali.
Hatua hiyo inalenga kuboresha mawasiliano na kuondoa changamoto ya kutokuelewana inayojitokeza pale wateja viziwi wanapofika kupata huduma katika vituo vya posta.
Akizungumza na wataalamu wa anuai za jamii kutoka ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora pamoja na Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, meneja wa shirika la posta mkoa wa Dodoma Dongwe Dongwe amesema uwepo wa wataalam wa lugha ya alama utaongeza ufanisi, usalama na usawa katika utoaji wa huduma.

Ameeleza kuwa kabla ya kuanza rasmi kwa matumizi ya wataalam hao shirika hilo litatoa mafunzo kwa watumishi wake kuhusu namna sahihi ya kuhudumia watu wenye ulemavu .
Kwa upande wake mkurugenzi msaidizi wa anuia za jamii kutoka ofisi ya Rais Menejimenti ya utumishi wa umma na utawala bora Mwanaamani Mtoro amesema serikali inaendelea kuweka mikakati ya kuhakikisha huduma za kidigitali zinafika kwa makundi yote ikiwemo watoto ili kuwajengea uwezo wa matumizi sahihi ya teknolojia wakiwa katika umri mdogo.
Nae mshauri muelekezi wa mradi wa DTP Caroline Ndosi amesema mradi huo unaunga mkono jitihada zote zinazolenga kujenga mifumo jumuishi ya huduma za umma kwa kutumia teknolojia rafiki kwa makundi yoyote ya kijamii.