Dodoma FM
Dodoma FM
14 January 2026, 2:05 pm

Hatua hii inakuja ili kukabiliana na changamoto ya baadhi ya wazazi kuwapeleka watoto wao mjini kufanya kazi za nyumbani, jambo ambalo limekuwa kikwazo katika kupata elimu kwa watoto waliofaulu kujiunga na shule za sekondari.
Na Victor Chigwada.
Wakati muhula mpya wa masomo 2026 umeanza hapo jana Januari 13, uongozi wa Kijiji cha Msanga wilayani Chamwino jijini Dodoma umeweka mkakati maalum wa kuhakikisha wanafunzi wote waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza wanaripoti shuleni.
Mwenyekiti wa kijiji hicho Bw.Hatibu Ally amesema kijiji hicho kimekuwa kikikabiliwa na changamoto ya wazazi kuwapeleka watoto wao mjini kufanya kazi za ndani wakisingizia ugumu wa maisha hali inayo pelekea wanafunzi hao kushindwa kuripoti shuleni wanapokuwa wamefaulu kujiunga na kidato cha kwanza.
Aidha ameongeza kuwa moja ya mikakati waliyoiweka kwa mzazi ambaye mtoto wake hataripoti shuleni atalazimika kulipa faini ambayo itatumika kununua vifaa mbalimbali vya shule .
Nao baadhi ya wananchi wa Msanga wamewasihi wazazi kuhakikisha wanawapatia watoto haki ya kupata elimu badala ya kuwageuza watoto kama mitaji.