Dodoma FM
Dodoma FM
22 September 2025, 4:32 pm

Jamii pia imeshauriwa kujitokeza katika kliniki za watoto ili kupata elimu zaidi kuhusu lishe bora na namna ya kuandaa milo ya watoto kwa njia salama na yenye mvuto.
Na Peter Mnunduma.
Afisa Lishe kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Bi. Vaillet Mrema, ameitaka jamii kuzingatia aina ya chakula wanachowapa watoto baada ya kufikisha miezi sita ili kuhakikisha ukuaji bora na afya njema katika hatua za awali za maisha.
Amesema kuwa ingawa maziwa ya mama yanaendelea kuwa muhimu hata baada ya kipindi hicho, watoto wanapaswa kuanza kupewa vyakula vya ziada vyenye virutubisho vinavyosaidia ukuaji wa mwili na akili.
Bi. Mrema ameongeza kuwa vyakula hivyo vinapaswa kuwa vya aina mbalimbali, vikiwemo uji wenye lishe, mboga za majani, matunda, mayai, samaki na maharage yaliyopondwa au kupikwa vizuri.
Aidha, amewataka wazazi na walezi kuandaa chakula kwa usafi ili kuepusha magonjwa ya tumbo kwa watoto na kuwa wavumilivu, kwani mtoto anaweza kuhitaji muda kuzoea ladha na muundo mpya wa chakula.