Dodoma FM
Dodoma FM
26 January 2026, 3:23 pm

Wazazi wameshauriwa kushirikiana walimu shuleni kufuatilia maendeleo ya watoto na kuanzisha kampeni za uhamasishaji kuhusu athari za kuolewa mapema kwa wasichana.
Na Anwary Shabani.
Imeelezwa kuwa baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakishindwa kumaliza masomo yao kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo umaskini, ukosefu wa msaada wa wazazi, na baadhi ya wasichana kuolewa mapema.
Wakizungumza na Dodoma FM, baadhi ya wananchi kutoka jijini Dodoma wamesema hali hii ni changamoto kubwa kwa jamii na taifa, ikihitaji ushirikiano wa wazazi, shule, na jamii kwa ujumla ili kuhakikisha kila mtoto anapata fursa ya kufanikisha elimu yake.
Wananchi hao wameeleza njia mbalimbali ambazo wazazi, walezi na jamii kwa ujumla wanaweza kuzitumia ili kuhakikisha wanafunzi hawakatishi masomo na wanafikia malengo yao ya kielimu.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Denis Gondwe, amesema kuwa halmashauri inaendelea kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha wanafunzi wanabaki shuleni, wanakuwa salama na wanahitimu masomo yao kwa lengo la kuwaandaa kuchangia katika uchumi wa Taifa.