Dodoma FM
Dodoma FM
20 November 2025, 2:14 pm

Dkt. Fransis ameipongeza serikali kwa kuendelea kuboresha huduma za afya na kusisitiza umuhimu wa kila mwananchi kuwa na bima ya afya ili kurahisisha upatikanaji wa matibabu pindi wanapohitaji huduma.
Na Anwary Shaban.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limethibitisha kuongezeka kwa magonjwa mbalimbali katika jamii, yakiwemo magonjwa yanayoambukiza na yasiyoambukiza kama vile homa ya ini, presha ya damu na ugonjwa wa kisukari.
Hayo yamesemwa leo jijini Dodoma na Dkt. Fransis Mbwilo kutoka Taasisi ya UMATI, wakati akizungumza kuhusu mwenendo wa afya katika jamii na sababu zinazochangia kuongezeka kwa magonjwa hayo.
Dkt. Fransis amesema kuwa Shirika la Afya Duniani limebainisha ongezeko kubwa la wagonjwa wa homa ya ini duniani, na hapa nchini hali hiyo inaendelea kujionesha kwa kiwango cha kutia wasiwasi. Ameeleza kuwa moja ya sababu zinazoongoza kwa homa ya ini kuenea kwa kasi ni matumizi makubwa ya pombe kupita kiwango kinachoshauriwa kiafya.
Aidha, ametoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya magonjwa hayo kwa kufika vituo vya afya kupata chanjo na kufanya uchunguzi wa mara kwa mara ili kujilinda na madhara yatokanayo na kuchelewa kugundua maradhi.