Dodoma FM
Dodoma FM
12 November 2025, 11:59 am

Hii ni kutokana na baadhi ya watembea kwa miguu kushindwa kutambua sheria za alama za barabarani jambo ambalo upelekea ajali za mara kwa mara.
Na Anwary Shaban.
Watumiaji wa barabara hususani watembea kwa miguu wameaswa kuzingatia sheria na alama za barabarani ikiwemo kutembelea upande wa kulia na kuzingatia vivuko salama wakati wa kuvuka barabara.
Sajenti Ester Makali kutoka Ofisi ya Mkuu wa kikosi cha Usalama barabarani dawati la elimu kwa umma mkoa wa Dodoma amewakumbusha watembea kwa miguu kuzingatia sheria za barabarani na kuacha matumizi ya simu wakati wa kuvuka barabara ili kupunguza ajali.
Taswira ya habari ya Dodoma Fm imezungumza na baadhi ya watembea kwa miguu kutoka eneo la Nyerer Square, ambapo wamesema changamoto kubwa inayowakabili ni kutokana na watumiaji wa vyombo vya moto kutokuzingatia alama za watembea kwa miguu.
Nao baadhi ya madereva katika jiji la Dodoma wameeleza jinsi wanavyochukua tahadhari ili kuwalinda watu wanaotembea kwa miguu.
Sajent Ester amehitimisha kwa kutoa wito kwa madereva na watembea kwa miguu kuhakikisha wanazingatia sheria na alama za barabarani zilizowekwa pindi wanapokuwa wanatumia barabara.