Dodoma FM

Bodaboda waomba kutambulika katika makundi ya kazi

21 August 2024, 6:36 pm

Picha ni baadhi ya Madereva Bodaboda wakiwa barabarani .Picha na Google.

Mwezi Februari mwaka 2023 thamani ya Pikipiki zilizonunuliwa nje ya Nchi zilifikia Dola Milioni 136.7 sawa na Shilingi Bilioni 319.87 kiwango hicho ni zaidi ya Bajeti ya Kilimo ya mwaka 2021/22 huku ikielezwa Vijana wengi waliokosa ajira kukimbilia katika kazi hiyo.

Na Fred Cheti.

Kazi ya Usafirishaji Abiria kupitia Usafiri wa Pikipiki maarufu kama Bodaboda ni moja kati ya kazi zinazotajwa kuinua Maisha ya Vijana kutokana na wengi wao kujiajiri kupitia shughuli hiyo.

Mbali na kazi hiyo kusaidia Vijana wengi kujipatia kipato ni Usafiri unaosaidia kuokoa muda kwa Watu pia ni Usafiri pendwa kwa baadhi ya Watu.

Lakini wafanyaji wa shughuli hiyo ambao ni Maafisa usafirishaji wana matamanio mengi katika kazi hiyo ikiwemo kutambulika rasmi kama kundi la Wajasirimali huku wakiomba Serikali kuangalia uwezekano wa kupatiwa Mikopo binafsi ya Fedha au vyombo vya Usafiri ili waweze kuongeza vipato.

Baadhi ya maafisa Usafirishaji hao wanasema kuwa iwapo watapata mikopo binafasi itakuwa sehemu ya kuinua kazi zao na Maisha kwa Ujumla.

Juni 13 mwaka 2021 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye ziara Mkoani Mwanza alipata nafasi ya kuzungumza na Maafisa usafirishaji maarufu kama Bodaboda ambapo aliwataka kuwekeza zaidi na si kuishia kuendesha Bodaboda za Watu wengine.

Katika kipindi kilichoishia mwezi Februari mwaka 2023 thamani ya Pikipiki zilizonunuliwa nje ya Nchi zilifikia Dola Milioni 136.7 sawa na Shilingi Bilioni 319.87 kiwango hicho ni zaidi ya Bajeti ya Kilimo ya mwaka 2021/22 huku ikielezwa Vijana wengi waliokosa ajira kukimbilia katika kazi hiyo.