Storm FM
Storm FM
22 August 2026, 1:07 pm

Polisi Jamii ilianzishwa Agosti 25, 2006 na IGP Mstaafu Said Mwema kwa lengo la kuimarisha ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na Jamii ambapo maadhimisho hayo yameenda sambamba na zoezi la uchangiaji wa damu wa hiari.
Na: Ester Mabula
Jeshi la polisi mkoa wa Geita leo Agosti 22, 2026 limeadhimisha miaka 20 ya kuanzishwa kwa Polisi jamii nchini kwa kuzindua Polisi Jamii Run Club yenye lengo la kuimarisha ushirikiano baina ya na Jeshi la polisi na wananchi kupitia michezo mbalimbali.
Akizungumza wakati wa maadhimsiho hayo yaliyofanyika katika viwanja vya shule ya msingi Kalangalala Manispaa ya Geita, Kamanda wa polisi mkoa wa Geita SACP Safia Jongo amesema dhana ya polisi Jamii imeendelea kuacha alama ya umoja na ushirikiano baina ya Jeshi la polisi na wananchi.

Mgeni rasmi ambaye ni mkuu wa mkoa wa Geita amesema ushirikiano baina ya Jeshi la polisi na wananchi ni muhimu kwani unaendelea kusaidia kuimarisha mapambano dhidi ya vitendo vya uhalifu nchini huku akilipongeza Jeshi la polisi mkoa wa Geita kwa maadhimisho hayo.

Akizungumza mara baada ya uzinduzi huo Kamishna msaidizi wa Polisi (ACP) Amina Kahando ambaye ni mkuu wa Polisi Jamii mkoa wa Geita amesema maadhimisho hayo yamehususha washiriki kutoka maeneo mbalimbali huku baadhi ya washiriki wakieleza umuhimu wa kushiriki katika maadhimisho hayo.
