Storm FM
Storm FM
26 August 2026, 11:00 am

Daraja hilo lina midomo tisa (9) na lina urefu wa mita 40 kukamilika kwake kumekuwa na manufaa makubwa kwa wananchi wa maeneo hayo.
Na Mrisho Sadick:
Wakazi wa Kata ya Lwamgasa wilayani Geita wameipongeza Serikali kwa kukamilisha ujenzi wa Daraja la Buziba Ilangasika hali ambayo imewaondolea changamoto kubwa wananchi ya usafirishaji wa mazao, bidhaa na wagonjwa.
Wakizungumza baada ya Mwenge wa Uhuru kukagua na kuzindua daraja hilo Agosti 26,2026 baadhi ya wakazi wa Kata hiyo wamesema katika eneo hilo kuna mto unapita uliokuwa unahatarisha maisha ya wananchi waliokuwa wanavuka kwenda upande wa pili lakini kwasasa imebaki historia.

Akitoa taarifa mbele ya Mwenge wa Uhuru Mhandisi wa TARURA Wilaya ya Geita amesema ujenzi wa Daraja la Buziba Ilangasika umegharimu shilingi milioni 637 na umekamilika kwa asilimia 100 huku Mbunge wa Jimbo la Busanda ambae ni Naibu Waziri wa TAMISEMI Dkt Jafari Seif amesema kukamilika kwa daraja hilo ni mkakati wa serikali ya awamu ya sita.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Wazo Mwang’onda, amewataka wananchi wa Lwamgasa kulitunza na kulilinda daraja hilo, kwa kuwa Serikali imetumia fedha nyingi kulijenga kwa lengo la kuboresha maisha ya wananchi na kurahisisha shughuli za kiuchumi.