Storm FM

Serikali yawawezesha wakulima pampu za umwagiliaji Geita

8 August 2026, 12:27 pm

Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye zoezi la kukabidhi pampu za umwagiliaji ofisi ya mkuu wa mkoa wa Geita. Picha na Mrisho Sadick

Pampu hizo zimegawanywa katika halmashauri tano ambapo Bukombe imepata 16, Chato 41, Geita DC 50, Mbogwe 20 na Nyang’hwale 14.

Na Mrisho Sadick:

Serikali kupitia tume ya taifa ya umwagiliaji imekabidhi pampu 141 za umwagiliaji zenye thamani ya shilingi bilioni moja kwa vikundi vya wakulima mkoani Geita hatua hiyo ikilenga kuongeza uzalishaji wa mazao na kuwawezesha wakulima kulima mwaka mzima.

Kaimu mkuu wa mkoa wa Geita aliyekatikati akikabidhi pampu ya umwagiliaji kwa mkuu wa wilaya ya Nyang’hwale. Picha na Mrisho Sadick

Mhandisi kutoka Tume ya taifa ya Umwagiliaji Mkoa wa Geita Boniface Mkita amesema jumla ya wakulima 1,389 watanufaika na mpango huo wakiwemo wanawake 369 na wanaume 1,020 nakwamba Pampu hizo zitatumika katika maeneo yenye vyanzo vya maji ikiwemo mito na maziwa na zina uwezo wa kumwagilia zaidi ya ekari 20 kwa saa moja.

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Geita Paskas Muragili amesema kupitia mpango huo uzalishaji wa mahindi unatarajiwa kuongezeka kutoka tani moja hadi tani 2.5 kwa ekari huku akisisitiza walengwa kuzitunza ili zitumike kwa muda mrefu.

Muonekano wa miongoni mwa pampu za umwagiliaji zilizokadhibiwa kwa wakulima mkoa wa Geita. Picha na Mrisho Sadick

Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita Mohamed Gombati amesema katika mpango huo ekari zaidi ya 2,092 zinatarajiwa kumwagiliwa nakwamba matumizi ya pampu hizo yataongeza uzalishaji wa mbogamboga kutoka tani sita hadi tani 10 kwa ekari moja.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale amesema pampu hizo zitawawezesha wakulima kuzalisha kwa mwaka mzima bila kutegemea mvua.

Ripoti ya Stori hii na Mrisho Sadick