Storm FM
Storm FM
7 June 2026, 4:05 pm

“Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa hatua hii naimani kabisa Tuzo hii itaongeza motisha kwangu katika kazi yangu” – Ester Mabula
Na: Mrisho Sadick
Mwandishi wa habari na mtangazaji wa kituo cha Redio cha Storm FM kilichopo mkoani Geita Bi. Ester Mabula, ameshinda tuzo ya mtangazaji bora wa redio 2026 katika tuzo za Malkia wa Dahabu zilizofanyika usiku wa Juni 06, 2026 katika ukumbi wa Golden social hall kata ya Bombambili, halmashauri ya manispaa ya Geita.
Tuzo hizo zimeratibiwa na muandaaji Bi. Cecilia Miraji na zimefanyika kwa mwaka wa tatu mfululizo ambapo zimekuwa zikitolewa ili kutambua na kuthamini jitihada za wanawake katika sekta mbalimbali ikiwemo uchumi, ujasiriamali, uchimbaji, habari nk
Wanawake mbalimbali ndani na nje ya mkoa wa Geita walihudhuria katika hafla hiyo ambapo Mgeni maalumu Mkuu wa mkoa wa Geita Mhe. Martine Shigela amewapongeza wanawake wote walioshinda tuzo hizo huku akiwasihi kuongeza juhudi katika kazi zao.
Mgeni rasmi, Marry Chatanda ambaye ni Mwenyekiti wa UWT Taifa amesema wanawake ni nguzo kuu katika maendeleo kuanzia ngazi ya familia hadi Taifa na kwamba wasikubali kukatishwa tamaa.
Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa tuzo hiyo, Ester Mabula amesema ataendelea kufanya kazi kwa juhudi na kwamba tuzo hiyo itakuwa ni chachu ya kuongeza weledi zaidi katika kazi yake.