Storm FM
Storm FM
17 May 2026, 4:07 pm

Jumla ya wanafunzi 55 walihitimu shuleni hapo ambapo wanafunzi 50 walifaulu na kujiunga na kidato cha kwanza na kupelekea kushika nafasi ya kwanza kwenye kata hiyo huku masomo yaliyofaulisha vizuri yakiwa ni Kiswahili, Sayansi na Uraia na maadili.
Na: Ester Mabula
Uongozi wa kata ya Nyanguku Manispaa ya Geita umefanya hafla ya kuipongeza Shule ya msingi Nyakato kwa kufanya vizuri katika matokeo ya darasa la saba mwaka 2025.
Diwani wa kata hiyo ambaye pia ni Naibu Meya Manispaa ya Geita Mhe. Elias Ngole amesema hafla hiyo ni kiashiria cha kuongeza juhudi zaidi na motisha kwa shule nyingine ili zifanye vizuri zaidi huku akiwapongeza walimu wa shule ya Nyakato kwa hatua hiyo.
Muwakilishi wa ofisi ya mkurugenzi Manispaa ya Geita Bi. Mariam John amesemea matokeo hayo ni kielelezo cha uongozi mzuri wa kata hiyo na kuwapongeza walimu wote kwa kazi nzuri ya kuwafundisha wanafunzi.

Akizungumza Afisa elimu kata ya Nyanguku Mwl. Innocent Damas na mwalimu mkuu msaidizi wa shule ya msingi Nyakato Charles Laurent wamesema mafanikio hayo yametokana na jitihada za makusudi na mikakati iliyowekwa na walimu ili kuongeza ufaulu.
Kata ya Nyanguku ina jumla ya shule tano za msingi ambazo ni shule ya msingi Sinamwendwa, shule ya msingi Nyanguku, shule ya msingi Nyakato, shule ya msingi Mwagimagi na shule ya msingi Kakonda.
