

10 May 2025, 1:54 pm
Suala la michango kwa ajili ya shughuli za maendeleo katika kijiji limewatibua baadhi ya wananchi nakukimbilia CCM kuomba utatuzi.
Na Mrisho Sadick:
Wakazi wa Kijiji Cha Kalebezo Kata ya Nyamirembe wilayani Chato Mkoani Geita wamekiomba Chama Cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Geita kuingilia kati sakata la baadhi ya wananchi kudai kukamatwa nakuuziwa mifugo yao baada ya kushindwa kulipa mchango kwa ajili ya ukamilishaji wa vyumba vya madarasa.
Wananchi hao wametoa kilio hicho Mei 09,2025 mbele ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Geita aliyefika katika Kijiji hicho kusikiliza nakutatua kero za wananchi ambapo mbali na changamoto hiyo wamekiomba chama hicho kuisukuma serikali juu ya ukamilishaji wa ujenzi wa Kituo Cha Afya Cha Kata hiyo ambao unadaiwa kusuasua.
Mwenyekiti wa Kijiji hicho amekiri kuwepo wa mchango huo ambao umefuata taratibu zote ikiwa ni pamoja na vikao halali vya Kijiji ili kuwanusuru wanafunzi na changamoto mbalimbali huku akikanusha taarifa za watu kukamatwa nakuuziwa mifugo yao kisa michango hiyo.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Geita Nicholaus Kasendamila amewataka wakazi wa kata hiyo kutokwamisha mipango waliyokubalina kwenye mikutano halali ya Kijiji kwa manufaa yao huku akiahidi kufuatilia suala hilo la ukamilishaji wa vyumba vya madarasa pamoja na Kituo Cha Afya Cha Kata hiyo.