Storm FM
Storm FM
17 April 2026, 2:03 pm

“Ni muhimu kujiweka katika mazingira yenye kuheshimika kwenye Jamii kwa kuzingatia nidhamu ambayo hiyo itasaidia hata kwenye kuongeza ufaulu wa wanafunzi” – DED Myenzi
Na: Ester Mabula
Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya manispaa ya Geita Ndg. Yefred Myenzi amewataka walimu kuzingatia nidhamu na maadili ya kazi akieleza kuwa ndiyo silaha kuu ambayo itasaidia kuongeza ufaulu kwa wanafunzi sambamba na kuweka hadhi ya mwalimu kwenye Jamii.
Ndg. Myenzi ameyasema hayo April 16, wakati akihutubia siku ya mwalimu iliyoandaliwa na idara ya elimu sekondari, halmashauri ya manispaa ya Geita iliyofanyika katika ukumbi wa shule ya sekondari ya wasichana Nyankumbu.

Maadhimisho ya siku hiyo yaliambatana na bonanza la michezo mbalimbali sambamba na utoaji wa zawadi mbalimbali kwa walimu na shule zilizofanya vizuri katika mitihani ya kitaifa, ambapo mwalimu wa somo la Kiswahili kutoka shule ya Ihanamilo Mwita Magige amekabidhiwa zawadi ya pikipiki kutokana na jitihada za kuongeza ufaulu katika somo lake.

Baadhi ya walimu, mkuu wa shule ya wasichana ya Nyankumbu Khadija Kayanda na mwalimu Festo Nteze kutoka shule ya Ihanamilo wamepongeza uwepo wa siku hiyo wakieleza itatoa motisha kwa walimu kufanya vizuri zaidi.
