Storm FM

Serikali yakabidhi gari la wagonjwa kituo cha Afya Iparamasa

13 August 2026, 1:58 pm

Gari la wagonjwa lililokabidhiwa kwa kituo cha Afya Iparamasa kwaajili ya kusaidia wananchi wa kijiji hicho. Picha na Ester Mabula

Serikali imeendelea kuboresha kituo cha Afya Iparamasa kwa kukarabati miundombinu mbalimbali ili kusaidia utoaji wa huduma za afya kwa wananachi.

Na: Ester Mabula

Kituo cha Afya Iparamasa kilichopo  wilaya ya Chato mkoani Geita kimekabidhiwa gari la wagonjwa (Ambulance) lenye zaidi ya shilingi milioni 300 lililotolewa na serikali ili kuweza kusaidia wagonjwa wa dharura katika eneo hilo.

Hafla ya kukabidhi gari hilo imefanyika Agosti 12, 2026 katika kituo hicho, akitoa taarifa mbele ya mgeni rasmi Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Chato Ndg. Mandia Kihio amesema mradi huo wa kituo cha Afya umegarimu jumla ya shilingi milioni 741 zilizotengwa na kutolewa na serikali ikiwemo Milioni 105 zilizotumika kwaajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba na Milioni 45 kwaajili ya kukamilisha ujenzi wa miundombinu ya maji kupitia mradi wa Wash.

Sauti ya mkurugenzi Ndg. Mandia Kihio
Muonekano wa Jengo la kituo cha Afya Iparamasa wilayani Chato mkoani Geita. Picha na Ester Mabula

Mgeni rasmi, Mbunge wa Jimbo la Chato Kusini Mhe. Paschal Lucas Lutandula amesema ataendelea kuwa karibu na wananchi wake na kutimiza ahadi za kutatua changamoto  alizotoa wakati wa kampeni  huku akiahidi kujenga jengo la watumishi wa kituo hicho.

Sauti ya mgeni rasmi, Mbunge Paschal Lutandula

Baadhi ya wananchi wameipongzea na kuishukuru serikali sambamba na mbunge wa jimbo hilo kwa kuweza kuwasaidia kwa kuwapatia gari la wagonjwa kwani hapo awali walikuwa wakiteseka na kutumia gharama kubwa kwenda katika maeneo mengine iwapo itatokea dharura kwa wagonjwa.

Sauti ya wananchi
Mwananchi Tabu Singili akizungumza na waandishi wa habari baada ya hafla ya kukabidhi gari (hawapo pichani). Picha na Ester Mabula