Storm FM

TASAF yatekeleza miradi 56 ya zaidi ya bilioni 5 wilaya ya Geita

16 September 2026, 6:41 pm

NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Regina Ndege akikagua mradi wa Jengo la utawala Shule ya Sekondari Fadhili Bucha. Picha na Mrisho Sadick

Manispaa ya Geita TASAF imetumia zaidi ya Shilingi bilioni 2.4 kutekeleza miradi 30 ikiwemo miradi 24 ya elimu na sita ya afya

Na Mrisho Sadick:

NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Regina Ndege amesema Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) umeendelea kuboresha huduma za msingi kwa wananchi kupitia utekelezaji wa miradi ya afya na elimu huku zaidi ya Shilingi bilioni tano zimetumika kutekeleza miradi 56 katika Halmashauri mbili za Wilaya ya Geita mkoani Geita.

Mhe. Ndege amesema hayo baada ya kutembelea na kukagua miradi iliyotekelezwa kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF ikiwemo mradi wa ujenzi wa jengo la utawala katika Shule ya Sekondari Fadhili Bucha na kueleza kuwa kupitia miradi iliyokamilika TASAF imesaidia wananchi zaidi ya milioni 1.3 huku zaidi ya kaya laki nne zikiwa zimeweza kufikia hatua ya kujitegemea nakwamba katika awamu inayofuata, Mfuko huo unalenga kuhudumia zaidi ya kaya laki tano.

Jengo la utawala katika shule ya sekondari Fadhili Bucha lililojengwa na TASAF. Picha na Mrisho Sadick

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF Oscar Maduhu amesema TASAF imeendelea kuwa na manufaa kwa wananchi kwa kusaidia kuboresha huduma za msingi na kuwawezesha kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiuchumi na kijamii.

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Fadhili Bucha wakiwa katika ziara ya Naibu Waziri Shuleni hapo. Picha na Mrisho Sadick

Akieleza utekelezaji wa miradi hiyo katika Halmashauri hizo mbili Mkuu wa Wilaya ya Geita Hashim Komba amesema katika Halmashauri ya Manispaa ya Geita TASAF imetumia zaidi ya Shilingi bilioni 2.4 kutekeleza miradi 30 ikiwemo miradi 24 ya elimu na sita ya afya huku katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita zaidi ya Shilingi bilioni 2.7 zimetumika kutekeleza miradi 26 ambayo inajumuisha miradi 19 ya elimu na saba ya afya.

Ripoti ya Stori hii na Mrisho Sadick