Storm FM
Storm FM
11 September 2026, 4:06 pm

Serikali imewapa viongozi dhamana ya kusimamia ustawi wa wananchi, hivyo hakuna sababu ya kero zinazoweza kutatuliwa katika ngazi za wilaya na mkoa kuendelea kuwaumiza wananchi
Na Mrisho Sadick:
Mkuu wa Mkoa wa Geita Alexander Mnyeti amewataka watendaji wa serikali na viongozi Mkoani Geita kuhakikisha wanatatua kwa wakati kero zinazowakabili wananchi huku akisisitiza kuwa dhamana waliyopewa na serikali inapaswa kuonekana kupitia huduma na utatuzi wa changamoto za wananchi.
Mnyeti ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na watendaji wa serikali viongozi wa dini pamoja na wawakilishi wa makundi mbalimbali katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita.

Amewataka wakuu wa wilaya na watendaji wengine wa serikali kusimamia ipasavyo utatuzi wa changamoto zinazojitokeza katika maeneo yao, ikiwemo malalamiko yanayohusiana na dhuluma katika maeneo ya uchimbaji wa madini.
Amesema sekta ya madini ina umuhimu mkubwa katika uchumi wa Mkoa wa Geita hivyo ni muhimu kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinafanyika kwa kuzingatia sheria, haki za wananchi na maslahi ya jamii zinazozunguka maeneo ya migodi.

Katika hatua nyingine amewataka viongozi kujiandaa mapema kukabiliana na uwezekano wa mvua kubwa za El Niño kwa kuyatambua maeneo hatarishi, hususan yale yanayokumbwa na mafuriko, na kuhakikisha wananchi wanaoishi mabondeni wanaondolewa mapema na kuhamishiwa maeneo salama.