Storm FM
Storm FM
27 April 2026, 9:37 pm

Shule ya Msingi Fulwe iliyoanzishwa mwaka 1,956 imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya uchakavu wa miundombinu ya majengo hali iliyokuwa ikiathiri mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi
Na Mrisho Sadick – Geita
Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuchangia maendeleo ya jamii baada ya kukabidhi madarasa mawili yenye thamani ya shilingi milioni 50 pamoja na madawati 30 katika Shule ya Msingi Fulwe iliyopo Kata ya Nzera Wilaya ya Geita.
Akizungumza katika hafla ya makabidhiano hayo Mbunge wa Jimbo la Geita Vijijini Joseph Musukuma amepongeza hatua ya CRDB akisema uwekezaji huo ni mfano bora kwa taasisi nyingine kushiriki kikamilifu katika kuboresha huduma za kijamii hususani elimu.

Sambamba na hayo Mbunge Musukuma ameahidi kuchangia shililingi milioni 30 yeye pamoja na familia yake kwa ajili ya kufanikisha ujenzi wa madara mengine mawili , amesema ubora na thamani ya majengo yaliyotekelezwa na CRDB unapaswa kuigwa na watendaji wa serikali katika kusimamia miradi ya maendeleo kwa gharama nafuu na zenye ufanisi.
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa CRDB ambae ni Mkurugenzi wa TEHAMA Edward Mpina amesema mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa sera ya uwekezaji kwa jamii ya benki hiyo, ambapo hutenga takribani asilimia 1 ya faida baada ya kodi kila mwaka kusaidia sekta mbalimbali za maendeleo ikiwemo elimu nakwamba itaendelea kufanya hivyo.

Aidha meneja wa CRDB Kanda ya Magharibi Jumanne Wagana ameongeza kuwa benki hiyo itaendelea kuona umuhimu wa kuwekeza katika elimu kama msingi wa maendeleo endelevu ya taifa nakwamba mradi huo utakuwa chachu ya kuongeza ufaulu kwa wanafunzi katika shule hiyo.

Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Leonard Amos na baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo Said Said na Jeviva Salala wameipongeza CRDB kwa msaada huo wakisema umeleta matumaini mapya ya kujifunza katika mazingira bora zaidi kwakuwa baadhi ya madarasa katika eneo hilo yamejengwa na wakoloni.