Storm FM

RC Geita akagua ujenzi wa Zahanati Nyabulolo na Imalampaka Geita DC

22 June 2026, 8:30 pm

Mkuu wa Mkoa wa Geita Martine Shigela akizungumza na wananchi baada ya ukaguzi wa miradi ya Zahanati. Picha na Mrisho Sadick

Mkuu wa Mkoa wa Geita akiwa katika Halmashauri ya wilaya ya Geita ametembelea nakukagua miradi mbalimbali ikiwemo ya afya na elimu ambapo ameridhishwa na kasi ya utekelezaji wa miradi hiyo.

Na Mrisho Sadick:

Zaidi ya Shilingi milioni 259 zimetumika kwenye ujenzi wa zahanati katika Vijiji vya  Nyabulolo na Imalampaka Halmashauri ya Wilaya ya Geita Mkoani Geita hatua inayotarajiwa kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi wa maeneo hayo.

Wakazi wa Vijiji hivyo wakizungumza baada ya Mkuu wa Mkoa wa Geita Martine Shigela kutembelea nakukagua maendeleo ya ujenzi wa miradi hiyo wamesema kukamilika kwa zahanati hizo kutawaondolea changamoto ya kutembea umbali mrefu kufuata huduma za afya katika maeneo mengine.

Muonekano wa maendeleo ya ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Imalampaka Geita DC. Picha na Mrisho Sadick

Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita Dkt Modest Burchard amesema mwezi wa nane mwaka huu miradi hiyo itakuwa imekamilika kwa ubora na kuanza kutoa huduma kwa wananchi wa Vijiji hivyo.

Mkuu wa Mkoa wa Geita Martine Shigela amesema Serikali imepanga kutumia bilioni tatu kutoka Uwajibikaji wa Makampuni kwa Jamii CSR katika Mgodi wa GGML kukamilisha miradi viporo ya maendeleo ikiwemo maboma ya zahanati, vituo vya afya na miundombinu mingine muhimu.

Muonekano wa ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Nyabulolo Geita DC. Picha na Mrisho Sadick
Ripoti kamili ya Stori hii na Mrisho Sadick