

6 June 2024, 10:22 am
Msongo wa mawazo ni miongoni mwa sababu zinazotajwa katika baadhi ya matukio kuwa chanzo cha maamuzi yasiyo sahihi ambayo hufanywa na watu kutokana na shida, taabu, dhiki, matatizo au changamoto zinazomkabili katika maisha ya kila siku.
Na: Amon Mwakalobo – Geita
Kijana Salehe Damian (23) mkazi wa kata ya Buseresere wilayani Chato mkoani Geita amefikishwa kwenye ofisi ya serikali ya mtaa wa Msalala road ulipo katika halmashauri ya mji wa Geita kwa tuhuma ya kuvua nguo hadharani huku akitishia kuua watu alioeleza kuwa anawadai chenji baada ya kununua pombe.
Tukio hilo limetokea Juni 04, 2024 ambapo Kamanda wa polisi jamii katika mtaa huo anayejulikana kwa jina la Tumaini Bitelela amesema alipigiwa simu na wauza pombe waliopo kwenye eneo hilo kuwa kuna mtu anatishia maisha ya watu na ambapo alichukua jukumu la kufika katika eneo hilo.
Kijana huyo amekiri kufanya hivyo na kueleza sababu kuwa ni akili yake imechanganyikiwa baada ya mpenzi wake aliyemtaja kwa jina moja la Joyce kufariki kwani alikuwa anampenda sana.
Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa huo Bwana Sostenes Kalist amewahimiza wananchi katika mtaa wake kuendelea kutoa taarifa ya uwepo wa vijana ambao wana dalili za kufanya uhalifu.