Storm FM
Storm FM
15 May 2026, 4:52 pm

Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira Tanzania (NEMC) lilianzishwa mwaka 1986 ambapo maadhimisho ya miaka 40 yanatarajiwa kufanyika Mei 30, 2026.
Na: Ester Mabula
Kuelekea maadhimisho ya miaka 40 ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira Tanzania (NEMC), Kanda ya Ziwa Victoria Magharibi imezindua kampeni ya upandaji miti zaidi ya 3,000 katika Mkoa wa Geita huku zaidi ya miti 40,000 ikitarajiwa kupandwa nchi nzima kama sehemu ya juhudi za utunzaji wa mazingira.
Akizungumza wakati wa zoezi la upandaji miti lililofanyika leo Mei 15, 2026 katika Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) mkoa wa Geita, Meneja wa NEMC Kanda ya Ziwa Victoria Magharibi, Mhandisi Boniphace Guni amesema tangu NEMC ianzishwe mwaka 1986 imeendelea kusimamia jukumu lake la msingi la kuratibu na kusimamia mazingira nchini.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo Dkt. Elfas Msenya kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Geita ameipongeza NEMC kwa kuendelea kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa utunzaji wa mazingira akieleza serikali itaendelea kuunga mkono jitihada zote za utunzaji wa mazingira.

Katika utunzaji na uhifadhi wa mazingira mkoani Geita Kampuni ya Geita Gold Minning Limited (GGML) imeendelea kushirikiana na serikali pamoja na NEMC ambapo akizungumza Meneja wa mazingira kutoka GGML Bw. Mhando Yusuph amesema wanaamini katika kutunza mazingira kupitia sera zinazoongoza shughuli za mgodi huo.
Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Chuo cha VETA Geita Sebastian Masigo amesema chuo hicho kimeendelea uzingatia kanuni bora za uhifadhi mazingira huku wanachuo wakipongeza hatua hiyo kuwa italeta tija pamoja na kuboresha mazingira ya chuo.
