Storm FM

Wananchi watakiwa kufanya mazoezi kuepuka magonjwa yasiyoambukiza Geita

22 June 2026, 7:20 pm

Kaimu katibu tawala wa mkoa wa Geita Herman Matemu aliyevaa njano akiwa katika picha ya pamoja kwenye Bonanza la michezo. Picha na Mrisho Sadick

Mazoezi ya mara kwa mara yana mchango mkubwa katika kupunguza hatari ya kupata magonjwa kama shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo pamoja na unene uliopitiliza.

Na Mrisho Sadick:

Wananchi Mkoani Geita wamehimizwa kufanya mazoezi kuwa sehemu ya maisha yao ya kila siku ili kukabiliana na ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza ambayo yanaendelea kuwaathiri watu wengi kwa uzembe wa kutofanya mazoezi na kuzingatia lishe bora.

Mratibu wa Magonjwa Yasiyoambukiza Mkoa wa Geita Dkt. Grory Temba akizungumza kwenye bonanza la afya lililoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita na kufanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Kalangalala Manispaa ya Geita amesema magonjwa hayo yameendelea kuwa changamoto huku idadi ya wagonjwa ikiongezeka kutokana na mabadiliko ya mtindo wa maisha usiofaa ikiwemo kutofanya mazoezi.

Kaimu katibu tawala wa mkoa wa Geita Herman Matemu aliyevaa njano akiwa katika picha ya pamoja kwenye Bonanza la michezo. Picha na Mrisho Sadick

Dkt. Temba amesema mazoezi ya mara kwa mara yana mchango mkubwa katika kupunguza hatari ya kupata magonjwa kama shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo pamoja na unene uliopitiliza, hivyo wananchi wanapaswa kuyapa kipaumbele kwa ajili ya kulinda afya zao.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita Safia Jongo amewataka wataalamu wa afya kuendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya magonjwa hayo ili kuongeza uelewa wa kukabiliana na magonjwa hayo.

Kaimu katibu tawala wa mkoa wa Geita Herman Matemu aliyevaa njano akiwa katika picha ya pamoja kwenye Bonanza la michezo. Picha na Mrisho Sadick

Naye Katibu wa Chama cha Soka Wilaya ya Geita Shafi Mwinyimvua amesema michezo na mazoezi ni nyenzo muhimu katika kuimarisha afya za wananchi ameziomba  taasisi za umma na binafsi kuendelea kuandaa mabonanza na matukio ya michezo yatakayosaidia kuhamasisha jamii kujali afya zao.

Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita  Herman Matemu amesema serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za utoaji elimu ya afya na kuhimiza wananchi kushiriki mazoezi mara kwa mara ili kujenga jamii yenye afya bora na nguvu kazi imara kwa maendeleo ya mkoa na taifa kwa ujumla.

Baadhi ya washiriki wa bonanza hilo wameeleza kufurahishwa na tukio hilo wakisema limewapa fursa ya kufanya mazoezi, kupata elimu ya afya na kufahamu namna ya kujikinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.

Ripoti kamili na Mrisho Sasdick