Storm FM
Storm FM
26 June 2026, 8:05 pm

Wilaya ya Nyang’hwale imeendelea
Wilaya ya Nyang’hwale imeendelea kusisitiza umuhimu wa kutoa mikopo kwa vikundi vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu ili kuimarisha uchumi
Na Mrisho Sadick:
Mkuu wa wilaya ya Nyang’hwale Mkoani Geita Grace Kingalame ameziagiza taasisi nunuzi za serikali wilayani humo kuhakikisha zinatenga asilimia 30 ya zabuni nakutoa kwa vikundi Vya Vijana , Wanawake na Watu wenye ulemavu vilivyokidhi vigezo.
Kingalame ametoa maagizo hayo baada ya kukabidhi mikopo ya asilimia 10 kwa vikundi 32 ,zaidi ya shilingi milioni 211 huku akivitaka vikundi hivyo kuhakikisha vinajisajili kwenye Mfumo wa Taifa wa Ununuzi wa Umma kwa njia ya Kielektroniki NeST ili kupata zabuni mbalimbali zinazotangazwa na serikali ndani na nje ya wilaya hiyo.
Katibu tawala wa wilaya hiyo Kaunga Amani amewataka wataalamu wa maendeleo kuhakikisha wanavifuatilia vikundi vyote vilivyopata mkopo huku Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo John Isack amevitaka vikundi hivyo kuhakikisha vinafanya marejesho ili kutoa fursa ya vikundi vingine kupata.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale Husna Toni amevihimiza vikundi hivyo kuongeza ubunifu katika shughuli zao za kiuchumi ili kuvutia masoko mapya, kuongeza thamani ya bidhaa na huduma zao, pamoja na kukuza biashara zao kwa ushindani zaidi.
Mikopo hiyo imetolewa katika robo ya nne ya mwaka wa fedha 2025/2026, hadi sasa zaidi ya shilingi milioni 879 zimetolewa kwa vikundi zaidi ya 118 wilayani humo, Baadhi ya wanufaika wa mikopo hiyo wameeleza kuwa imechangia kwa kiasi kikubwa kuboresha shughuli zao za uzalishaji.
