Storm FM
Storm FM
30 June 2026, 4:09 pm

Jumla ya shilingi milioni 200 imetolewa na Mgodi wa GGML kupitia CSR kwa mwaka 2025/2026 ili kufanikisha utekelezaji wa mpango huo kwa kuzingatia vipengele vya uraghibishi, mafunzo kwa wakufunzi, mafunzo kwa watekelezaji na gharama za uendeshaji.
Na: Ester Mabula
Halmashauri ya manipaa ya Geita kwa kushirikiana na Mgodi wa GGML wamezindua afua ya unyunyiziaji viuadudu katika mazalia ya mbu ikiwa ni hatua inayolenga kupunguza kiwango cha maambukizi ya ugonjwa wa Malaria katika halmashauri ya manispaa ya Geita.
Akitoa taarifa ya mpango huo mbele ya mgeni rasmi, Mratibu wa Malaria manispaa ya Geita Mtashubirwa Nestory amesema gharama za utekelezaji wa afua hiyo ni shilingi milioni 200 ambayo imetolewa na mgodi wa GGML huku Mganga mkuu wa manispaa ya Geita Dkt. Fredrick Mugarula akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika mapambano ya Malaria kwani inalenga kudhibiti chanzo cha mazalia ya mbu.

Mgeni rasmi mkuu wa wilaya ya Geita Mhe. Hashim Komba amesema dhamira ya serikali ni kuendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo ili kupunguza maambukizi hadi kufikia Malaria 0 ifikapo 2030 huku akitoa takwimu za maambukizi ya Malaria katika manispaa ya Geita.
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa GGML Dkt. Kiva Mvungi amewaomba wananchi kutoa ushirikiano ili kufanikisha utekelezaji wa afua hiyo huku Dkt. Mtemi Rusasa ambaye ni meneja wa Afya wa GGML amesema kupitia mpango huo jumla ya kata 13 zenye mitaa 78 zitafikiwa ili kunyunyuzia dawa hiyo.

Baadhi ya wahudumu wa afya ngazi ya jamii Azory Barosha na Sarah Revocatus wakieleza kuwa mpango huo utasaidia kuimarisha mapambano dhidi ya Malaria sambamba na kujenga uelewe kwa wananchi juu ya ugonjwa wa Malaria.
