

16 April 2025, 3:00 pm
Jeshi la polisi katika mkakati wa kukabiliana na changamoto ya vitedo vya ukatili kwa watoto Mkoani Geita
Na Mrisho Sadick:
Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limeanza oparesheni ya kuwakamata watoto wanaozurura mitaani nyakati za usiku na kuwawajibisha wazazi wao ili kukabiliana na changamoto ya vitendo vya ukatili ikiwemo vya ulawiti kwa watoto hao.
Kauli hiyo imetolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita kamishna msaidizi mwandamizi wa Polisi Safia Jongo wakati akizungumza na wakazi wa Kata ya Katoro wilayani Geita ikiwa ni mwendelezo wa kampeni ya Elimu ya Polisi Jamii inayofadhiliwa na Mgodi wa GGML.
Kwa upande wake mrakibu msaidizi wa jeshi la polisi kutoka makao makuu dawati la jinsia na ulinzi wa mtoto Wilfred Willa amewataka wazazi na walezi kuwajibika kwa watoto ikiwemo kujenga utamaduni wa kuwakagua watoto hao mara kwa mara.
Baadhi ya wakazi wa Kata hiyo wamepongeza hatua ya Jeshi la Polisi kuanzisha oparesheni hiyo itakayo kuwa msaada kwa watoto hao huku wakiwaomba wazazi kuhakikisha wanawajibika kwa watoto wao ili kukabiliana na changamoto ya vitendo vya ukatili kwa watoto.