Storm FM
Storm FM
18 August 2026, 6:56 pm

Awali walikuwa wakitoza kati ya shilingi 300 hadi 500 kwa abiria kwa safari za umbali mrefu, lakini kwa sasa wanatoza kati ya shilingi 500 hadi 1,000 kwa umbali wa wastani, jambo ambalo wanasema limeongeza kipato chao.
Na Mrisho Sadick:
Waendesha baiskeli za daladala katika Manispaa ya Geita mkoani Geita wamesema wameendelea kunufaika na kupanda kwa bei ya mafuta kwa kuwa hatua hiyo imewafanya wananchi wengi kuhamia kwenye usafiri wa baiskeli kutokana na gharama nafuu.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya waendesha baiskeli hao wamesema tofauti na vyombo vya moto, baiskeli zao hazitumii mafuta hivyo kupanda kwa bei ya mafuta kumesababisha pikipiki na bajaji kuongeza nauli hali iliyowafanya wananchi wengi kuchagua baiskeli.

Kwa mujibu wa William John aliyeanza kufanya kazi hiyo tangu mwaka 2012 amesema ongezeko la wateja pamoja na nauli limewasaidia kupata kipato cha kuendesha familia zao na kukidhi mahitaji ya kila siku, huku wakiiomba jamii kuendelea kutumia usafiri huo kwa kuzingatia usalama barabarani.