Joy FM
Joy FM
4 August 2026, 10:43

Kwa matokeo hayo ya asilimia 100 ya ufaulu wa kidato cha sita, Halmashauri ya Mji Kasulu inaendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuimarisha sekta ya elimu na kuzalisha wahitimu wenye uwezo wa kuchangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla
Na Hagai Ruyagila
Halmashauri ya Mji Kasulu Mkoani Kigoma imeendelea kufanya vizuri katika sekta ya elimu baada ya wanafunzi wa kidato cha sita waliofanya mtihani wa taifa mwaka 2026 kufaulu kwa asilimia 100.
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kasulu, Mwl. Vumilia Julius Simbeye, wakati akizungumza na Radio Joy FM mjini Kasulu.
Mwl. Simbeye amesema matokeo ya mwaka huu yameonyesha mafanikio makubwa, ambapo wanafunzi wengi wamepata madaraja ya A na B, hali inayoonesha kuimarika kwa kiwango cha elimu na kuongeza matarajio ya halmashauri kupata wastani wa daraja la A katika matokeo ya kitaifa.
Amesema mikakati na juhudi zilizowezesha kupatikana kwa matokeo hayo mazuri zitaendelea kutumika kuimarisha ufaulu wa wanafunzi wa kidato cha nne na kidato cha pili ili Halmashauri ya Mji Kasulu iwe miongoni mwa halmashauri zinazofanya vizuri zaidi katika Mkoa wa Kigoma na nchini kwa ujumla.
Aidha, Mwl. Simbeye ametoa wito kwa wazazi na walezi kushirikiana na serikali kwa kufuatilia maendeleo ya watoto wao shuleni, kuhakikisha wanapata mazingira mazuri ya kujifunzia na kuwahamasisha kujituma katika masomo.
Baadhi ya wazazi na walezi waliozungumza na Radio Joy FM wamesema wataendelea kufuatilia kwa karibu maendeleo ya watoto wao kitaaluma, wakiamini ushirikiano kati ya wazazi na walimu ni nguzo muhimu ya kuongeza ufaulu na kuwajengea wanafunzi mustakabali mzuri wa maisha.