Joy FM

DC Uvinza asikiliza kero za wananchi atakaa uimarishaji utoaji wa huduma

29 June 2026, 08:53

Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mh. Dinah Mathamani akiwa katika mkutano wa kusikiliza kero za wananchi, Picha Mwandishi wetu

Serikali ina wajibu wa kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na changamoto zao zinatatuliwa kwa wakati na mojawapo ya njia zinazosaidia kufanikisha jambo hili ni viongozi kuwafikia wananchi moja kwa moja, kusikiliza maoni yao na kutafuta suluhisho la matatizo yanayowakabili

Na Mwandishi wetu

Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mh. Dinah Mathamani, amefanya ziara katika Kata ya Uvinza kwa lengo la kusikiliza na kutatua kero zinazowakabili wananchi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mh. Dinah Mathamani akiwa katika mkutano wa kusikiliza kero za wananchi, Picha Mwandishi wetu

Akizungumza katika mkutano huo, Mh. Dinah amesema changamoto ya mabasi kutofika stendi ya mwisho imepata ufumbuzi kufuatia kuanza rasmi kwa shughuli katika Stendi ya Wilaya ya Uvinza. Ameagiza mabasi yote yaliyosajiliwa kutoa huduma hadi Uvinza kuhakikisha yanafika katika stendi hiyo kuanzia leo.

Kwa upande wa maendeleo ya kijamii, Mkuu wa Wilaya amewahakikishia wananchi kuwa Serikali itatenga na kuandaa eneo linalofaa kwa ajili ya shughuli za michezo na burudani, ili kukuza ustawi wa jamii na vipaji vya vijana.

Aidha, amewataka maafisa wa Jeshi la Polisi kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia haki, sheria na misingi ya utawala bora ili kuimarisha uhusiano mwema kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

Mwakilishi kutoka Polisi akizungumza wakati wa Mkutano wa Mkuu wa Wilaya Uvinza Dinnah Mathamani wa kusikiliza kero za wananchi, Picha na Mwandishi wetu

Akizungumzia mgogoro wa ardhi unaoikabili Kata ya Ruchugi, Mh. Dinah ameahidi kuwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya itashirikiana na mamlaka husika kuhakikisha mgogoro huo unapatiwa suluhisho la kudumu kwa maslahi ya wananchi wote.

Baadhi ya wananchi wakiwa kwenye mkutano wa Mkuu wa Wilaya Uvinza Dinnah Mathamani, Picha na Mwandishi wetu