Joy FM
Joy FM
27 April 2026, 12:17

Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni moja ya matukio muhimu zaidi katika historia ya Tanzania, ulioweka msingi wa taifa moja lenye umoja, amani na mshikamano na Muungano huu ulianzishwa tarehe 26 Aprili 1964, ukiziunganisha nchi mbili zilizokuwa huru kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Na Hagai Ruyagila
Mkuu wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, Kanali Isaac Mwakisu, amewataka wananchi wa Wilaya hiyo kuendelea kudumisha na kuuenzi Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ili kuimarisha amani iliyopo nchini.
Kanali Mwakisu ametoa wito huo wakati wa zoezi la upandaji miti lililofanyika katika Shule ya Msingi Kimobwa Halmashauri ya Mji Kasulu, ambapo jumla ya miti 150 imepandwa ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 62 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Amesisitiza umuhimu wa Muungano huo kwa maendeleo ya taifa, na kueleza kuwa utunzaji wa mazingira ni msingi muhimu kwa ustawi wa maisha ya wananchi.
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi CCM wilaya ya Kasulu, Mbelwa Chidebwe amesema wao kama Chama Cha kilichopo madarakani, wataendelea kuisimamia serikali iendelee kudumisha Muungano.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji Kasulu, Mwl.Vumilia Julius Simbeye amesema upo umuhimu mkubwa wa kuuenzi Muungano ulioasisiwa na viongozi wetu.

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Kimobwa ameahidi kusimamia na kuitunza miti hiyo ili iweze kusaidia kuboresha mazingira ya shule.