Joy FM

Mahakama tatu za mwanzo zazinduliwa Kigoma

19 June 2026, 20:44

Ni baadhi ya viongozi wakiwa katika hafla ya uzinduzi wa mahakama tatu, Picha na Timotheo Leonard

Uzinduzi wa mahakama hizo kunatajwa kusogeza huduma karibu na wananchi ambao walitumia muda mwingi kufuata huduma za mahakama mbali na maeneo yao

Na Timotheo Leonard

Mahakama za Mwanzo za Bangwe, Herujuu na Manyovu zimezinduliwa rasmi leo Juni 19, 2026 mkoani Kigoma, hatua inayolenga kusogeza huduma za sheria na haki karibu zaidi na wananchi wa maeneo hayo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, mgeni rasmi ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Augustine Karichuba Rwizile, amesema uwepo wa mahakama hizo unapaswa kuwa chachu kwa watendaji wa mahakama kuendelea kutenda haki kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji ili kulinda heshima ya mhimili wa mahakama.

Sauti ya Jaji Rwezile
Baadhi ya mahakimu wakiwa wakiwasili viwanja vya mahakama, Picha na Timotheo Leonard

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Simoni Sirro, amesema mahakama hizo zitasaidia kupunguza gharama za usafiri kwa wananchi waliokuwa wakisafiri umbali mrefu kufuata huduma za mahakama, huku akiahidi kuwa serikali itaendelea kushirikiana na mhimili huo katika kuboresha utoaji wa haki.

Awali, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Yusuph Kasuka, amesema miradi ya ujenzi wa mahakama hizo tatu umegharimu zaidi ya shilingi bilioni mbili, ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali za kuimarisha miundombinu ya utoaji haki nchini.

Muonekano wa mahakama ya Buhigwe ikiwa ni miongoni mwa mahakama zilizozinduliwa, Picha na Timotheo Leonard

Baadhi ya wananchi waliohudhuria hafla hiyo wameipongeza serikali kwa kukamilisha miradi hiyo, wakisema itasaidia kusogeza huduma za mahakama karibu na wananchi na kupunguza mlundikano wa kesi katika maeneo yao.