Joy FM
Joy FM
31 July 2026, 16:02

Msaada huo ni sehemu ya Jshi hilo kuendelea kuimarisha ukaribu na ushirikiano kwa jamii
Na Hagai Ruyagila
Jeshi la Polisi Wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma limetoa msaada wa vitu mbalimbali ikiwemo sabuni, mafuta ya kujipaka na kanga nguo, kwa wagonjwa waliolazwa katika Hospitali ya Mlimani iliyopo Halmashauri ya Mji Kasulu, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na jamii.
Akizungumza wakati wa kukabidhi zawadi hizo, Kamishna Msaidizi wa Polisi na Mkuu wa upelelezi na makosa ya jinai mkoa wa kigoma Alfred Kasolo, amesema Jeshi la Polisi ni sehemu ya jamii, hivyo limeona umuhimu wa kurejesha shukrani kwa wananchi linaowalinda kwa kuwafariji wagonjwa waliolazwa hospitalini.

Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mlimani, Editha Yohana Vubuka, ambaye pia ni Muuguzi Mfawidhi wa hospitali hiyo, amesema msaada huo utasaidia kupunguza baadhi ya changamoto zinazowakabili wagonjwa na hospitali kwa ujumla. Aidha, amelishukuru Jeshi la Polisi kwa kuonyesha upendo na huruma kwa wagonjwa kupitia msaada huo.

Baadhi ya wagonjwa waliopokea zawadi hizo wameeleza kufurahishwa na hatua ya Jeshi la Polisi ya kuwafikia na kuwapa zawadi hizo, wakisema kitendo hicho kinaonyesha kuwa jeshi hilo linathamini na kushirikiana na jamii hata katika nyakati za matatizo.
