Joy FM
Joy FM
2 September 2026, 13:14

Mwenge wa Uhuru ni miongoni mwa alama muhimu za kitaifa, ambazo hutumika kuhamasisha wananchi kuhusu masuala ya maendeleo, amani, umoja, uzalendo na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo nchini.
Na Hagai Ruyagila
Mkuu wa wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, Kanali Isaac Mwakisu, ameongoza kikao cha kamati maalum cha maandalizi ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru, unaotarajiwa kuwasili wilayani humo Septemba 9, 2026.
Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa shule ya sekondari Bogwe na kimejumuisha Halmashauri mbili za wilaya ya Kasulu ikiwemo Halmashauri ya Mji Kasulu na Halmashauri ya wilaya ya Kasulu.

Katika kikao hicho, Kanali Mwakisu amepokea taarifa za maandalizi kutoka kwa kamati mbalimbali zinazohusika na maandalizi ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru, ambapo amewataka madiwani na watendaji wa kata kuendelea kuwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi katika mapokezi ya Mwenge sambamba na kuzingatia usafi kabla na baada ya mkesha.
Mratibu wa Mwenge wa Uhuru Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu Thomas Kisaka anazungumzia baadhi ya shughuli ambazo Mwenge wa Uhuru utazindua na kutembelea katika halmashauri hiyo.

Na hapa Mratibu wa Mwenge wa Uhuru Halmashauri ya Mji Kasulu Nurfus Aziz Ndee anazungumzia baadhi ya shughuli ambazo Mwenge wa Uhuru utakazo tembelea na kuzindua katika halmashauri hiyo.
Baadhi ya washiriki wa kikao hicho, wakiwemo viongozi wa vyama vya siasa, madiwani, taasisi binafsi na taasisi za umma, wamesema maandalizi yanaendelea vizuri na wametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru.
