Joy FM

JAI yazindua zoezi la uchangiaji damu salama Kasulu

22 July 2026, 17:22

Baadhi ya wanakikundi cha Kiislamu JAI waliojitokeza kuchangia Damu salama, Picha na Emmanuel Kamangu

Uchangiaji wa damu salama ni moja ya matendo muhimu ya kibinadamu yanayochangia kuokoa maisha ya watu wengi na damu ni rasilimali muhimu ambayo haiwezi kutengenezwa viwandani, hivyo hupatikana kupitia watu wanaojitolea kuchangia

Na Emmanuel Kamangu

Kikundi cha Kiislamu cha JAI wilayani Kasulu, mkoani Kigoma, kimezindua zoezi la uchangiaji wa damu salama katika Hospitali ya Mji wa Kasulu Mlimani, likiwa na lengo la kuongeza upatikanaji wa damu na kuokoa maisha ya watu wenye uhitaji.

JAI ni jumuiya inayojihusisha na huduma za kibinadamu, ikiwemo kuwahudumia wagonjwa, yatima na wajane. Kupitia zoezi hilo, wanachama wa jumuiya hiyo wameendelea kuonesha moyo wa kujitolea kwa kuchangia damu ili kusaidia kuokoa maisha ya wagonjwa mbalimbali, wakiwemo wajawazito wanaohitaji huduma za dharura.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa zoezi hilo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Dkt. Nangi William, ambaye alikuwa mgeni rasmi, aliihamasisha jamii kujitokeza kwa wingi kuchangia damu salama. Aidha, aliipongeza JAI kwa kuendelea kuonesha moyo wa kujitolea na kushiriki katika shughuli zinazogusa maisha ya wananchi.

Mganga mkuu Dkt. Nangi Williamu katika hafla ya uchangiaji damu akizungumza na wana JAI waliojitokeza katika zoezi hilo, Picha na Emmanuel Kamangu

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa JAI wilayani Kasulu, Sheikh Abdulrahman Nyamugenda, alisema kuwa miongoni mwa shughuli kuu zinazotekelezwa na jumuiya hiyo ni utoaji wa misaada mbalimbali, ikiwemo huduma za damu, matibabu kwa watu wasiojiweza, pamoja na kuwasaidia wahitaji bila ubaguzi wa dini, kabila au asili.

Mratibu wa kikundi cha kiislamu JAI Shekhe Abulahaman Nyamgenda akisoma taarifa za maendeleo ya kikundi hicho katika utekelezaji wa matendo ya huruma katika jamii, Picha na Emmanuel Kamangu

Naye Mlezi wa JAI, Sheikh Alhaji Masoud, alitoa wito kwa jamii kuendelea kuishi kwa upendo, mshikamano na huruma kwa kuwajali watu wenye mahitaji mbalimbali, akisisitiza kuwa kusaidiana ni msingi muhimu wa maendeleo ya jamii.

Awali, akisoma risala ya jumuiya hiyo, Katibu wa JAI wilayani Kasulu, Bi. Aisha Rubeni, amesema kuwa hadi sasa jumuiya hiyo imefanikiwa kutoa huduma mbalimbali kwa wagonjwa 3,164. Alitoa wito kwa Serikali na jamii kuendelea kushirikiana na kuiunga mkono JAI ili iweze kuendelea kutoa huduma kwa makundi yenye uhitaji katika jamii.