Joy FM

Watoto wenye umri chini ya miaka mitano kupatiwa vyeti vya kuzaliwa bure Kigoma

4 October 2023, 08:59

Waziri wa Katiba na Sheria Dkt Pindi Chana akikabidhi cheti cha kuzaliwa kwa mama alipata cheti wakati wa uzinduzi, Picha na Tryphone Odace.

Wakazi wa mkoa wa Kigoma wamefurika katika viwanja vya mwanga manispaa ya Kigoma Ujiji, ili kusajili na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano.

Na, Tryphone Odace

Wazazi na Walezi wenye Watoto chini ya Umri wa Miaka mitano wametakiwa kujitokeza kwa wingi katika Ofisi za Watendaji Kata na Katika vituo vya kutolea huduma za afya kwa lengo la kusajili na kupata vyeti vya kuzaliwa.

Waziri wa Katiba na Sheria Nchini Tanzania Dkt. Pindi Chana amesema hayo wakati akizindua Mpango wa Kusajili na Kutoa Vyeti vya kuzaliwa chini ya Miaka 5 Mkoani Kigoma.

Katika Uzinduzi huo umefanyikia katika Uwanja wa Mwanga Community Centre Manispaa ya Kigoma Ujiji ambapo Waziri Chana amesema zoezi hilo la Usajili na Kutoa vyeti vya kuzaliwa litafanyika katika Ofisi za Watendaji Kata na vituo vya kutolea afya bure huku akiwataka Wananchi wenye watoto wenye Umri huo kujitokeza.

Waziri wa Katiba na Sheria Dkt pindi chana akizungumza na wananchi wa Mkoa wa Kigoma akizungumza na wananchi wa Mkoa wa Kigoma, Picha na Tryphone Odace

Akitoa Salamu katika Mkutano huo Mkuu wa Wilaya  ya Kigoma Salum Hamis Kali Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa amesema zaidi ya Watoto laki tatu  396,000 wanatarajiwa kusajiliwa na kupata vyeti vya kuzaliwa.

Hata hivyo katika uzinduzi huo, Mamia ya wakazi wa mkoa wa Kigoma wamefurika katika viwanja vya mwanga manispaa ya Kigoma Ujiji, ili kusajili na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano, huku wakiomba serikali kuweka wepesi na kurahisisha upatikanaji wa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto.

Afisa mtendaji wa Kata ya Mwanga Kusini akiwa katika zoezi la kusajili watoto ili wapate vyeti vya kuzaliwa, Picha na Tryphone Odace

Wakizungumza wakati wa zoezi la uzinduzi wa mpango wa usajili wa kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano, baadhi ya wananchi wamesema, kabla ya mpango huo walilazimika kukosa vyeti vya watoto kutokana na vigezo rukuki na kutumia mda mwingi kufuatilia mchakato wa upatikanaji wa vyeti.