Joy FM

RAS Kigoma ataka elimu ya ukatili iendelee kutolewa kwa jamii

12 December 2025, 18:11

Washiriki wa Kongamano la kilele cha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia lililofanyika Mjini Kasulu, Picha na Hagai Ruyagila

Wadau mbalimbali wa masuala ya ukatili wa kijinsia kwa kushirikiana na Serikali wametakiwa kuendelea kutoa elimu na mikakati ya kukabiliana na vitendo vya ukatili

Na Hagai Ruyagila

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Hassan Rugwa, amewataka wadau wa maendeleo kuendelea kutoa elimu ya malezi kwa jamii, hususan elimu ya kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia, ili kuhakikisha wazazi na walezi wanalea watoto wao katika misingi sahihi itakayochangia ukuaji bora wa mtoto.

Akizungumza katika kongamano la kilele cha Kampeni ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia lililoshirikisha watumishi wa umma, taasisi binafsi na viongozi wa dini, katika ukumbi wa chuo cha ualimu Kasulu TTC Rugwa amesema ushirikiano wa karibu kati ya wadau mbalimbali utaongeza ufanisi katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia na kuimarisha uelewa wa pamoja ndani ya jamii.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Hassan Rugwa, Picha na Hagai Ruyagila

Amesema kuwa malezi sahihi pamoja na kuzingatia maadili mema kutoka kwa wazazi na walezi ni msingi muhimu wa ukuaji mzuri wa mtoto.

Sauti ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Hassan Rugwa

Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Kigoma, Msafiri Nzunuri, amesema vitendo vya ukatili wa kijinsia vimeendelea kupungua kutokana na juhudi za serikali na wadau wa maendeleo kutoa elimu kwa jamii kupitia kampeni na programu mbalimbali za uhamasishaji.

Sauti ya Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Kigoma, Msafiri Nzunuri
Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Kigoma, Msafiri Nzunuri, Picha na Hagai Ruyagila

Mkuu wa dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Kigoma, Mrakibu msaidizi wa Jeshi la Polisi Michael Mjema amesema licha ya kupungua kwa baadhi ya matukio ya ukatili, lakini vitendo hivyo bado vipo, hivyo jeshi la polisi kitengo cha dawati la jinsia na wadau wa maendeleo wameendelea kutoa elimu ili kuvitokomeza kabisa

Sauti ya Mkuu wa dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Kigoma, Mrakibu msaidizi wa Jeshi la Polisi Michael Mjema

Baadhi ya wananchi walioshiriki katika kongamano hilo akiwemo Theresia Mohamed na Lazaro Simon wamesema wanaotoa taarifa na wapo ambao hawatoi taarifa hivyo elimu endelevu kwa jamii ni muhimu ili kupunguza au kutokomeza vitendo vya ukatili, jambo litakalosaidia watoto kupata malezi bora kutoka kwa wazazi na walezi.

Sauti ya Baadhi ya wananchi walioshiriki katika kongamano hilo akiwemo Theresia Mohamed na Lazaro Simon
Washiriki wa Kongamano la kilele cha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia lililofanyika Mjini Kasulu, Picha na Hagai Ruyagila

Kongamano la kilele cha Kampeni ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia limebebwa na kaulimbiu isemayo “Tuungane, Kutokomeza ukatili wa kijinsia mitandaoni”