Joy FM
Joy FM
11 July 2026, 12:13

Wananchi na wafanyabiashara katika masoko mbalimbali yaliyopo katika Halmashauri ya Mji wa Kasulu Mkoani Kigoma wametakiwa kuchukua tahadhali ya moto wawapo katika shughuli zao za kila siku ili kuepuka kuwa chanzo cha majanga ya moto
Na Hagai Ruyagila
Zaidi ya vibanda tisa katika Soko la Muganza, lililopo Kata ya Mganza, Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma, vimeteketea kwa moto kufuatia ajali inayodaiwa kusababishwa na mafuta ya mawese yaliyokuwa yakichemshwa na mmoja wa wafanyabiashara sokoni hapo.

Baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo, lililotokea leo Julai 10, 2026, katika soko la Muganza wamesema mfanyabiashara huyo alidaiwa kuchemsha mafuta ya mawese ndani ya kibanda chake, kisha kufunga mlango na kuondoka huku mafuta yakiendelea kuchemka. Hali hiyo inadaiwa kusababisha moto ulioenea kwa kasi na kuteketeza vibanda hivyo pamoja na mali mbalimbali za wafanyabiashara.
Akizungumza baada ya kutembelea eneo la tukio, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji Kasulu, Mwalimu Vumilia Julius Simbeye, amewapa pole wafanyabiashara waliopata hasara kutokana na janga hilo.

Aidha Mwl, Simbeye amewashauri wafanya biashara hao kujenga vibanda kwa kutumia matofali na vifaa vinavyostahimili moto ili kupunguza athari za namna hiyo.
Mkuu wa Wilaya ya Kasulu, Kanali Isaac Mwakisu, amemtaka mtu anayehusishwa na chanzo cha moto huo kujisalimisha katika Kituo cha Polisi kwa ajili ya uchunguzi na hatua za kisheria. Amesisitiza kuwa uzembe unaohatarisha maisha na mali za wananchi hautavumiliwa.

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na Wananchi wamefanikiwa kuudhibiti moto huo na kuzuia usienee katika maeneo mengine ya soko, huku tathmini ya kina ya hasara iliyosababishwa ikiendelea kufanywa.
