Joy FM
Joy FM
2 June 2026, 14:31

Damu ni rasilimali muhimu katika huduma za afya kwa kuwa hutumika kuokoa maisha ya wagonjwa wanaopoteza damu kutokana na ajali, upasuaji, kujifungua na magonjwa mbalimbali
Na Emmanuel Kamangu
Mkoa wa Kigoma umeweka lengo la kukusanya chupa 21,000 za damu salama kila mwaka ili kuhakikisha wananchi wanaopoteza damu kutokana na sababu mbalimbali wanapata huduma kwa wakati na kuokoa maisha yao.
Akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Kasulu katika hafla maalumu ya uchangiaji damu iliyowakutanisha wakazi kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Dkt. Damas Kayera, alisema kuwa mkoa huo umeendelea kuvuka lengo hilo kila mwaka kutokana na mwitikio mkubwa wa wananchi wanaojitokeza kuchangia damu.
Dkt. Kayera aliwashukuru wananchi wa Mkoa wa Kigoma kwa moyo wao wa kujitolea na kuendelea kuchangia damu salama, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha kiwango kikubwa cha upendo, utu na mshikamano miongoni mwao, hasa katika kuwajali watu wanaohitaji damu kwa ajili ya matibabu.
Kwa upande wao, baadhi ya wananchi wa Wilaya ya Kasulu waliojitokeza kuchangia damu walieleza kuwa kitendo hicho ni sehemu ya ibada na huduma kwa jamii, kwani damu wanayochangia huwasaidia watu wenye mahitaji mbalimbali ya kiafya.
Wananchi hao pia walitoa wito kwa jamii kuendelea kuhamasika na kushiriki katika uchangiaji wa damu salama, wakisisitiza kuwa kujitolea kuchangia damu ni hatua muhimu inayookoa maisha ya watu wengi na kuimarisha huduma za afya katika jamii.