Joy FM

Wanaume watakiwa kuripoti matukio ya ukatili Kigoma

8 July 2026, 11:42

Pichani ni Mkuu wa Dawati la jinsia na watoto Mkowa Kigoma ASP Michael Mjema, Aifsa ustawi wa jamii Mkoa wa Kigoma na Afisa maendeleo ya jamii pamoja na watangazaji wa Redio Joy Fm, Picha na Joy Fm

Ukatili wa kijinsia ni tatizo linaloathiri wanawake, wanaume na watoto katika jamii na kwa muda mrefu, jamii imekuwa ikielekeza zaidi macho kwa ukatili dhidi ya wanawake, hali iliyowafanya baadhi ya wanaume wanaopitia ukatili kushindwa kutoa taarifa kwa hofu ya kudharauliwa au kutokuaminiwa.

Na Filbert Gabriel

Wanaume Mkoani Kigoma wametakiwa kutoa taarifa za matukio ya ukatili yanayotokea katika jamii badala ya kukaa kimya, ili kuchangia kujenga kizazi bora cha baadaye na kuendeleza juhudi za kumlinda na kumlea mtoto wa kiume.

Akizungumza katika mahojiano maalumu yaliyofanyika kwenye studio za Radio Joy Fm, Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Kigoma, Efeta Msiga, amesema baba ndiye nguzo ya familia, hivyo ana wajibu wa kujilinda, kuilinda familia yake na kutoa taarifa za vitendo vya ukatili wa kijinsia vinapotokea.

Sauti ya Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Kigoma, Efeta Msiga

Naye Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Kigoma, Amina Kaniki, amesema wanaume hukumbwa na aina mbalimbali za ukatili ikiwemo ukatili wa kihisia na kimwili huku akihimiza kujitokeza hadharani na kutoa taarifa wanapofanyiwa au wanaposhuhudia vitendo vya ukatili.

Sauti ya Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Kigoma, Amina Kaniki

Kwa upande wake,  Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Kigoma, ASP Michael Mjema, amesema wanaume wanapaswa kufika katika ofisi za Dawati la Jinsia na Watoto kutoa taarifa za vitendo vya ukatili wanapovikumbana navyo au kushuhudia wengine wakifanyiwa, badala ya kuwa na mtazamo kwamba huduma za dawati hilo zinawanufaisha wanawake pekee.

Sauti ya Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Kigoma, ASP Michael Mjema

Mkoa wa Kigoma unaendelea kukabiliwa na changamoto ya matukio ya ukatili dhidi ya watoto wa kiume, hususan vitendo vya ulawiti ambavyo, katika baadhi ya matukio, hufanywa na watu wa karibu na waathirika na hali hiyo inaelezwa kuwa tishio kwa ustawi wa watoto hao na maendeleo ya familia pamoja na jamii kwa ujumla.